Mchaka Zaidi

Thursday, May 28, 2015

Huyu Ndo Zitto Kabwe Ninayemfahamu Ambaye CHADEMA Wameamua Kumpaka Matope


Sijawahi  kuwa  Mwanachama  wa  Chama  cha  ACT-Wazalendo  na sijafikiria  kujiunga  na  chama  hicho. Nilishawahi  kuwa  Mwanachama  mtiifu  wa  chama  cha  Demokrasia  na  maendeleo (Chadema)

Nikiwa  ndani  ya CHADEMA  nimewahi  shiriki  katika  harakati  nyingi  zote  zikiwa  na  lengo  la  kukikuza  chama  ambacho  niliamini  ndo  mkombozi  wa  kweli  wa  mtanzania.

Bahati  mbaya  sikuwa  sahihi, nilikosea  kukiamini  chama  hicho  ambacho  idadi  kubwa  ya  viongozi  wake  ni  mahafidhina.

Nikiwa  ndani  ya  siasa, nimefanikiwa  kujuana  na  wanasiasa  wengi  wakubwa  kwa  wadogo, mmoja  wao  ni  kiongozi  mkuu  wa  ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe.

Namjua  Zitto, nafahamiana  naye  vizuri, ni  mmoja  wa  wanasiasa  wasomi, wenye  siasa  safi  ambaye  mara  zote  kauli na  hoja  zake  zimetaliwa na  busara  na  nia  ya  kulijenga  taifa, siwezi  kusema  si  mbinafsi  moja  kwa  moja  lakini  nina  imani  nae  kubwa  kuwa  si  mbinafsi.

Zitto  ameweza  kuzimudu  siasa  safi  za  taka  zilizokuwa  zikiendeshwa  ndani  na  nje  ya  chadema  kabla  ya  kuhamia  ACT- Wazalendo.Ameweza  kupambana  na  kupenya  kwenye  changamoto  nyingi  za  kisiasa  hasa  siasa  hizi  za  kuwa  na  chama  kimoja  kikongwe  na  chenye  nguvu  nchini  na  nje  ya  nchi.

Sote  tunaijua  CCM  ni  chama  chenye  wanachama  na  viongozi  wanaoijua  siasa, wanaweza  kukibadili  chama  hicho  wakati  wowote, chama  hiki  kikuu  nchini  ni  kama  kinyonga, kinabadiilika  kulingana  na  mazingira  na  wakati.

CCM  kinapanga  vyema  karata  zake, kina  propaganda  zenye  kuwiana  na  ukweli  tofauti  na  ilivyo  kwa  upinzani  ambao  wanadanganya  wananchi  mpaka  wanajidanganya  wao  wenyewe.

Zitto  ameweza  kupenya  kote  huku  na  ndio  maana  leo  hii,  Zitto  anaposulubiwa  hata  CCM  kinaumia  na  kumhurumia, kwa  sababu  wanamjua  mwanasiasa  huyu  kijana  ni  mtu  wa  namna  gani.

Kama  si  uimara  wa  Zitto  huenda  angeshaanguka  maana  wapo  watu  na  vyama  vilivyotupwa  nje  ya  siasa  kutokana  na  kukosa  misingi  ya  mapambano  ya  siasa  za  aina  zote.

Hata  hivyo  chadema  kimefika  hapo  kilipo  pamoja  na  mambo  mengine  mchango  wa  Zitto  unahusika  kwa  kiwango  kikubwa.

Katibu  mkuu  wa  chadema  Dr. Wilbroad  Slaa  kwa  kushirikiana  na  Zitto  walieweza  kukifikisha  chama  hapo  kilipo, hilo  haliepukiki  na  anayekataa  ana  chuki  zake  binafsi.
Zitto  akiwa  mchanga  kisiasa  lakini  mwenye  maono  alichanga  karata  zake  vyema, akashiriki  kukitoa  chama  kutoka  kuwa  na  wabunge  11  hadi  kukifikisha  hapa  kilipo, ambapo  leo  kuna  zaidi  ya  wabunge 40.
Historia  ya  Chadema  haiwezi  kukamilika  bila  ya  kumhusisha Zitto  katika  mafanikio  yake  huku  akipambana  kwa  karibu  sana  na  Dr. Slaa, na  mbunge  wa  Kawe, Halima  Mdee  ambaye  kwa  bahati  mbaya  amejikuta  akivurugwa  na  wapambe.
Chadema  ya  Zitto  akiwa  kama  Naibu  katibu  mkuu  Bara, waliweza  kukidhibiti  CUF  na  Hamad  Rashid  ambaye  alikuwa  kinara  ndani  ya  bunge.
CUF  ilikuwa  na  hoja  dhaifu  na  mikakati  isiyotekelezeka  pamoja  na  kauli  mbiu  za  hatari  za  mapanga  shaa,Interehamwe  na  Saigon.
Chadema  ya  Zitto  na  Dr  Slaa  walikuwa  wakitoa  hoja  zenye  mashiko, walikuwa  moto  mkali  ndani  ya  bunge, hakuna  aliyeacha  kuwasikiliza  watu  hao  wanapopata  nafasi  ya  kuzungumza.Bunge  la  9  lilikuwa  ni  moto  wa  kuotea  mbali.
Bunge  hilo  lilileta  mapinduzi  makubwa  ya  kiungozi  na  kiutendaji  serikalini.Mikataba  mibovu  ilichambuliwa,Sakata  la  EPA  iliiibuka, mgodi  wa  Buzwagi  nao  ulipewa  nafasi  na  masikini  walipiganiwa.

Chama  kikanawiri  na  kushamiri  hadi  kufikia  leo  kuwa  na  wabunge  40, ajabu  ni  kwamba  baadhi  ya  viongozi  wa  chama  hicho  wamesahau  mema  yote  ya  Zitto  badala  yake  wanashiriki  kwenye  harakati  chafu  za  kumchafua.

Wanataka  kuiaminisha  jamii  kuwa  Zitto  ni  Msaliti, kwamba  anapaswa  kutukanwa, kusimangwa  na  kubezwa. Zitto  huyu  anayejua  kupanga  karata  leo  hii  amekuwa  adui  na  msaliti  wa  chadema, chama  alichojiunga  nacho  akiwa  kinda!

Dhambi  hii  ya  ubaguzi  waliyoifanya  Chadema  itawarudia, hawatapona  kamwe, hawatabaki  salama, wataparanganyika  tu, nawaombea  heri  wasifike  huko  ingawa  dhambi  ya  ubaguzi  haiishi.

Kama  nilivyotangulia  kusema  hapo  juu, namjua  Zitto, nimefanya  nae  kazi  ni  mmoja  wa  waliokuwa  viongozi  kipenzi  cha  watu  wa  rika  na  kada  zote  ndani  ya  chama  hicho.

Alipendwa  naa  viongozi  wa  ngazi  ya  chini  Chadema, alikuwa  ni  mtu  wa  kujishusha  na   kuwasikiliza  viongozi  waliochini  yake.Hata  kama  aliyoelezwa  yalikuwa  nje  ya  uwezo  wake  hakuyapuuza.

Tofauti  yake  na  viongozi  wakubwa  wa  chadema, yeye  alikuwa  akifika  kwenye  mikutano  hata  akute  watu  wachache  hakuwa  akiacha  kuhutubia  na  kuwapa  moyo.

Alikuwa  akiyatumia  mazingira  hayo  ya  watu  wachache  kusimulia  baadhi  ya  visa  vyake  vya  kisiasa, wakati  huo  ndo  wanajenga  chama.

Naamini  anakikumbuka  kisa  hiki, kwamba  yeye  na  Mdee  walikwenda  mahali  na  kukuta  watu  wachache.Hwakuacha  kuhutubia, walihutubia, lakini  ajabu  hao  watu  wachache  waliokuwepo  walikuwa  wakiendelea  na  harakati  zao, wengi  wao  walikuwa  wakinunua  ndizi  mbivu......Kwa   maana  nyingine  hawakuwa  wakisikilizwa.

Alichokifanya  ni  kumuomba  Mdee  akazinunue  zile  ndizi  zote  ili  watu  wakose  cha  kununua  na  badala  yake  wageuke  kuwasikiliza.

Hata  hivyo, mpango  wao  huo  haukufanikiwa, kwani  kila  mtu  aliyekuwa  pale  aliendelea  na  mambo  yake. Chakufurahisha  Zitto  na  Mdee  hawakukata  tamaa, walipambana  kuwashawishi  watu  wakielewa  chama.Leo  hii  chama  kikifika  eneo  lile  lile  watu  wanakanganyana  ili  kumsikiliza  kiongozi  wa  chama  anayezungumza  hata  kama  anaongea  pumba.

Zitto alikuwa  mtu  wa  kujichunga  sana  katika  matamshi  yake, hakuwa  akiongea  bora  aongee, alikuwa  akiongea  yanayopaswa  kuongelewa  kwa  wakati  huo  na  kwa  wakati  stahiki.

Mwandishi: Joseph Yona ( 0713802226)


Chanzo: Mpekuzi blog

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.